Ukiwa ni mtu wa kutaka kurudishiwa shukrani pale unaposaidia basi utaumia sana kisaikolojia.
Waswahili wanasema shukrani ya punda ni mateke.
Kazi yako kubwa iwe ni kufanya kazi yako na siyo kusubiri shukrani. Wewe toa bila kuwa na matarajio ya kupokea.
Pata picha kuku anavyotimiza wajibu wake wa kutaga na kutoa mayai, ulishawahi kumuona akilalamika hata siku moja? Lakini anataga kwa sababu ni wajibu wake kufanya hivyo na asipofanya hivyo anajikuta anaumia yeye mwenyewe.
Ng’ombe alishawahi kuacha kutoa maziwa kwa sababu watu wanakunywa maziwa na hawampi shukrani?
Vipi kuhusu jua, kila siku linawaka na linatusaidia kwenye mahitaji yetu mbalimbali lakini ulishawahi kulisikia likisema watu hawana shukrani nawapa nishati kila siku lakini hawanishukuru?
Ni wangapi wanaamka salama kila siku bila hata ya kushukuru? Lakini ulishawahi kusikia Mungu ameacha kazi yake ya kuwapa watu mahitaji yao ya kila siku licha ya kutomshukuru kwa mema yote ambayo anaendelea kuwatendea?
Sasa wewe ni nani ambaye kila unachotaka kufanya unataka watu wakutambue na kukushukuru kwa kile ulichofanya?
Hatua ya kuchukua leo; fanya kazi yako na timiza wajibu bila kusubiri kushukuriwa na wengine.
Jaribu kufikiria ni vingapi unavipata bure kwa njia tu ya asili lakini husemi asante?
Usiwe na manung’uniko moyoni kwamba unafanya kitu lakini huoni hata anayekupa shukrani yoyote ile.
MUHIMU;
Kama bado hujajiunga na kundi la wasapu la Mimi ni Mshindi jiunge leo kwani kuna maarifa mengi unayakosa ambayo sikushirikishi hapa.
Kujua ni maarifa gani hayo na jinsi ya kujiunga nitumie ujumbe wasapu kwa namba 0717101505. Kupata vitabu vizuri vya kujisomea kwa lugha ya kiswahili wasiliana kwamba namba 0717101505.
Rafiki Na Mwalimu Wako, Afisa Mhamasishaji Mkuu (CIO)Chief Inspiration Officer.
Mwl. Deogratius Kessy
0717101505 au 0767101504
https://kessydeo.home.blog