Usichague kuwa mtu asiyekuwa na thamani. Kuwa mtu wa thamani au kutokuwa mtu wa thamani ni kuchagua.
Usichague kuishi maisha ya juu ya kipato chako. Haijalishi una kipato kikubwa au kidogo unatakiwa kuishi chini ya kipato chako.
Usichague kuishi bila kuweka akiba. Weka akiba mara nyingi uwezavyo kwani akiba itakuja kukusaidia hapo baadaye na uzuri wa akiba huwa haiozi.
Usichague kuishi bila kufanya uwekezaji wowote ule. Kwani bila kuwekeza unakua huna tofauti na mtu ambaye hakui na hajui kule anakoenda. Sehemu unayopata kwenye kipato chako hakikisha unaiwekeza kwanza. Kula kipato chako chote ni kula mbegu na sijawahi kuona mkulima makini anakula mbegu na wewe usifanye hivyo.
Usichague kuishi bila kusoma. Soma, soma, soma. Njia rahisi ya kujifunza vitu vingi kwa muda mfupi ni kwa njia ya kusoma vitabu. Soma vitabu, usikose kusoma katika siku yako unayopata nafasi ya kuishi.
Usichague kuishi bila kufanya mazoezi. Fanya mazoezi kila siku, mara kwa mara kwa namna yoyote ile fanya mazoezi kwa sababu mwili wako uko katika mwendo lakini wewe unataka uende kinyume na asili na madhara ya kuipinga asili ni makubwa hivyo jitahidi kufanya hivyo.
Usichague kuishi bila kuwa na mahusiano mazuri na watu wengine. Ishi na watu vizuri, wapende kisha upendo utakurudia. Wasiliana vizuri na watu na ongea vizuri na watu kwa sababu kile unachotaka utakipata kupitia watu wenyewe.
Usikubali kuishi bila kusamehe. Kuchagua kuishi bila kusamehe ni kuchagua kufa. Kiasili hakuna anayeweza kumaliza siku yake bila kero yoyote ile. Wako wanaotukwaza na kutuumiza hivyo tusipochagua kusamehe na kuachilia yale yanayotusibu utajikuta unashindwa kufanya kazi zako za maana. Siyo kazi yako kuwabeba watesi wako, mwachie Mungu apambane na watesi wako wewe fanya kile unachopaswa kufanya tu.
Hatua ya kuchukua leo; usichague kuishi bila kuchukua hatua yoyote ile kiakili, kimwili na kiroho. Utatu wa maisha uko kwenye maeneo haya matatu akili, mwili na roho. Kila siku kua zaidi ya jana kwenye maeneo hayo.
Maisha ni kukua kila siku, usichague leo yako iwe kama jana. Ishi kitofauti ili upate vitu tofauti, mazoea yatakupa kitu kile kile ambacho unakipata mara kwa mara.
Muhimu;
kama bado hujajiunga na kundi la wasapu la mimi ni mshindi ajiunge leo kwani kuna maarifa mengi unayakosa ambayo sikushirikishi hapa.
Kujua ni maarifa gani hayo na jinsi ya kujiunga bofya hapa au nitumie ujumbe wasapu kwa namba 0717101505. Kupata vitabu vizuri vya kujisomea kwa lugha ya kiswahili bonyeza hapa.
Rafiki Na Mwalimu Wako,
Mwl. Deogratius Kessy
0717101505/0767101504
deokessy.dk@gmail.com //
Asante Sana
©Kessy Deo