Habari mpendwa rafiki na msomaji wa mtandao wa Kessy Deo? Ni matumaini yangu kuwa u buheri wa afya. Hongera kwa zawadi ya siku hii ya leo ambapo leo ni siku ya pili katika mwaka 2017 tunapaswa kuutumia vizuri muda wetu kwani ukishapotea hatuwezi kuurudisha tena.
Mpendwa msomaji, usikubali siku yako ipite bila hata ya kufanya jambo lolote kwenye maisha yako. Usiendelee tena kuwa katika utamaduni wa kulalamika kwani mwaka 2016 tulishajifunza sana kuwa wewe ndio mkurugenzi wa maisha yako. Pambana na maisha yako mpaka upate kile unachokitaka na usiogope kuona unapitia mawimbi mbalimbali kwani hakuna mtu ambaye hapitii changamoto hapa duniani.

Hivyo basi, napenda kutumia nafasi hii tena kukualika katika somo letu la leo ambapo leo tutakwenda kujifunza namna ya kuepuka kuwa msambaza sumu kwenye maisha yako. Nakusihi sana rafiki uambatane pamoja nami mpaka mwisho wa somo letu la leo.
Mpendwa msomaji, hakuna kitu kibaya kama kuwa msambaza sumu katika maisha yako. Wasambaza sumu wamekuwa ni wengi wanaondelea kuua watu kutokana na sumu zao wanazo sambaza. Wasambaza sumu ni wale watu wanaoongelea mambo chini chini badala ya kwenda kumwambia mtu husika kuwa jambo Fulani haliko sawa yeye anaanza kuanzisha maneno ya chini chini.
Kwa mfano, unafanya kazi katika taasisi Fulani sasa kuna mambo anayofanya kiongozi wako wa eneo la kazi siyo mazuri na hayapendezi. Sasa wewe badala ya kwenda kumwambia kuwa ndugu unaenda vibaya na kumwambia ukweli unaanza kumwaga sumu za majungu, umbea na kurusha makombora ya kila aina unayoyajua kwa watu wa pembeni badala ya mhusika mkuu.
SOMA;Maeneo Matatu (03) Muhimu Ya Kufanyia Usafi Ndani Ya Siku Kumi Zilizobaki Kabla Ya Mwaka 2016 Kuisha
Namna gani unaweza kuepuka kuwa msambaza sumu kwenye maisha yako? Njia rahisi ya kuepuka kuwa msambaza sumu kwenye maisha yako ni kwenda kumwambia ukweli mhusika moja kwa moja. Ukimwona jirani, ndugu, rafiki na jamaa anaenda mrama nenda kamfate akiwa mwenyewe na mueleze ukweli badala ya kuanza kusambaza sumu za unafiki.
Mpendwa msomaji, wasambazaji sumu katika maisha yetu ndio watu wanaochangia kuharibu na kuvunja uhusiano wetu ulijengeka imara hapo awali. Waswahili wanasema heri mchawi kuliko mnafiki. Hivyo kuwa huru kwa kusema ukweli pale mambo yanapokuwa yanaenda vibaya katika jamii yako kwa kumfuata mhusika na siyo kuanza kusambaza sumu.
Hatua ya kuchukua leo, kama ulikuwa ni mtu hodari wa kurusha sumu za makombora ya umbea, unafiki, majungu, kusengenya na n.k acha mara moja. Mwenzako akiwa ameenda mrama mfuate na mueleze ukweli yeye mwenyewe badala ya kuanza kumwaga sumu kwengine itakayokuja kuwadhuru na wengine hatimaye kuvunja uhusiano ulio bora miongoni mwetu.
SOMA;Hii Ndiyo Kazi Inayolipa Kwa Sasa Kuliko Kazi Nyingine Zote
Kwahiyo. Mpendwa msomaji na rafiki yangu inatupasa kuepuka kuwa sehemu ya usambazaji sumu katika maisha yetu. Kataa kabisa kuwa sehemu ya watu wanaosambaza sumu eneo la kazi ulilopo. Kwa kufanya hivyo tunakuwa tunayengeneza mazingira salama ya kuishi duniani.
Mwisho, usisahu pia kumshirikisha na mwenzako makala hii nzuri uliyosoma leo. Pia, Hakikisha unapenda ukurasa wetu wa facebook kwa maarifa zaidi na kupata kitabu cha kujisomea bonyenza hapa.
Nakutakia kila la heri katika haya uliyojifunza leo. Endelea kutembelea mtandao huu kujifunza kila siku. Asante sana.
Rafiki na mwalimu wako,
Deogratius Kessy
0717101505 /0767101504 au deokessy.dk@gmail.com
Leave a comment